Friday, March 23, 2012

Sosholojia ya Qur'an 2: Je Mwanadamu Ni Mwanajamii Kwa Asili?

Assalamu Alaikum Wa Rahmatu Allah Wa Barakatuh

Ndugu zangu katika imani! katika sehemu ya kwanza ya mada hii, tuliangalia maana ya jamii na michanganuo yake. Na leo hii nawasilisha kwenu sehemu ya pili ya mada hii katika kuangalia iwapo mwanadamu ni mwanajamii kwa asili au la.

Hoja inayohusu mambo yanayohusika au yaliyosababisha kuibuka kwa maisha ya kijamii kwa binadamu, imekuwa ikiibuliwa kutoka nyakati za zamani. Je mwanadamu amezaliwa na silika ya kupenda kushirikiana na wengine (gregariousness)? Yaani, je kwa asili aliumbwa kama sehemu ya kitu kikubwa (ujumla), akiwa na wito ndani ya maumbile yake unaomtaka kuungana na kitu hicho kikubwa (ujumla)? Au hakuumbwa kuwa kiumbe anayependa kushirikiana na wengine (gregarious), lakini nugvu na utambuzi wa nje vikamlazimisha kuishi maisha ya pamoja? Kwa maneno mengine, je yeye kwa asili ana mwelekeo au silika ya kuishi kwa uhuru, na kwamba ana mwelekeo wa kutokubali aina yoyote ya wajibu na mipaka ambayo amewekewa, japokuwa mipaka hiyo inaweza kuwa muhimu kwa maisha ya kijamii? Je, kweli amejifunza kutokana na uzoefu kwamba hakuna mtu anayeweza kuishi peke yake, na hivyo akalazimika kusalimu amri mbele ya mipaka iliyowekwa na maisha ya kijamii? Au, ingawa yeye si kiumbe anayependa kushirikiana na wenzake (gregarious) kwa asili, sababu iliyomshawishi kukubali maisha ya kijamii haikuwa ya lazima, au angalau ulazima huo sio sababu pekee? Au, ni kwa hukmu ya akili yake na kwa kufanya ukokotozi ndiyo akafikia uamuzi wa kwamba ni kwa ushirikiano na maisha ya pamoja ndipo anapoweza kufurahia zawadi ya kuumbwa kwake na hivyo akachagua kuishi katika ushirikiano na wanadamu wengine? Kutokana na hali hii, hoja hiyo inaweza kuwekwa katika njia tatu:

1.Je mwanadamu ni mwanajamii kwa asili?

2.Je mwanadamu ni mwanajamii kwa kulazimishwa?

3.Je mwanadamu ni mwanajamii kwa hiari yake na uchaguzi wake mwenyewe?

Kwa mujibu wa nadharia ya kwanza, maisha ya kijamii ya mwanadamu ni sawa na ushirikiano wa mwanaume na mwanamke katika maisha ya ndoa; kila mmoja wa washirika ameumbwa kama sehemu ya kitu kizima, na, kwa asili, anatamani na anataka sana kuungana na kitu hicho kizima. Kwa mujibu wa nadharia ya pili, maisha ya kijamii ni kama ushirikiano, kama vile mkataba kati ya nchi mbili ambazo zikiwa moja moja haziwezi kujitetea dhidi ya adui anayewakabili wote, na jambo hilo linawalazimisha kufanya makubaliano ya kushirikiana. Kwa mujibu wa nadharia ya tatu, maisha ya kijamii ni sawa na ushirikiano wa mabepari wawili, ambao huibua usuhuba wa kibiashara, kilimo au uzalishaji unaolenga kupata faida kubwa.

Kwa msingi wa nadharia ya kwanza, sababu kuu ya mwanadamu kuwa katika maisha ya kijamii ni ya asili ambayo imo katika maumbile na silika yenyewe ya mwanadamu. Kwa msingi wa nadharia ya pili, sababu kuu ni kitu kingine kabisa kutoka nje ya asili na silika ya mwanadamu na ambacho hakitegemei silika hiyo. Na kwa mujibuwa wa nadharia ya tatu, sababu kuu inayohusika na maisha ya kijamii ni akili na na kipawa cha mwanadamu mwenyewe.

Kulingana na maoni ya kwanza, udamisi/uanajamii (sociability) ni lengo kuu na la wote ambalo kwa asili mwanadamu anataka, anatamani na anagombania kulifikia. Kwa mujibu wa nadharia ya pili, udamisi/uanajamii (sociability) ni jambo la kawaida na limetokea tu kama ajali, ni jambo la pili na la ziada na sio lengo la awali na la msingi. Kwa mujibu wa nadharia ya tatu, udamisi/uanajamii (sociability) ni matokeo ya akili na uwezo wa mtu wa kuhoji na kudadisi.

Baada ya kuziangalia hizo nadharia tatu kuhusu uanajamii wa mwanadamu, ni upi msimamo wa Qur’an Tukufu katika hizo nadharia? Je ni nadharia ya kwanza, ya pili au ya tatu? Ili kuyajibu maswali haya, basi ungana nami katika sehemu ifuatayo ya mada hii.

Nakutakia siku njema…

No comments:

Post a Comment